Wednesday, March 4, 2015

Mkurugenzi wa TGNP, Lilian Liundi
Mkurugenzi wa TGNP, Lilian Liundi

Wanawake wataka mafanikio zaidi

WAKATI Tanzania ikiungana na mataifa mengine duniani kusherehekea Siku ya Wanawake, Mtandao wa Jinsia Tanzania (TGNP), umeainisha changamoto kadhaa zinazowakabiri wananwake nchini. Anaandika Sarafina Lidwino... (endelea).
Akizungumza na waandishi wa habari leo katika maadhimisho ya miaka 20 ya azimio la Ulingo wa Beijing, Mkurugenzi wa TGNP, Lilian Liundi amesema, siku hii hukutanisha wanaharakati wote wanaotetea haki za wanawake ili kujadili mafanikio na changamoto na jinsi ya kukabiliana nazo.
Liundi amesema, pamoja na mafanikio waliyoyapata hususani katika nyanja za kisiasa ya kuongezeka kwa viongozi wanawake, lakini bado kuna mapungufu katika uwezeshaji katika uongozi wao.
Amesema, mbali na kuongezeka kwa shule, bado hazikidhi mahitaji, majengo yapo lakini waalimu ni wachache na wengi hawana ujuzi, mabweni hakuna, umbali mrefu unaosababisha wasichana kupata mimba.   
Kwa mujibu wa Liundi, Serikali imejitahidi kujenga vituo vya afya, lakini changamoto iliyopo ni wahudumu hakuna wala dawa. Hivyo waathirika wakubwa ni wanawake, haswa wakati wa kujifungua, hukosa huduma na kupoteza maisha.
Lihundi amesema, mzigo wa majukumu unamwelemea sana mwanamke, hivyo kukosa muda wa kushiriki katika shughuri za kimaendeleo na uchumi.
Ameongeza kuwa bado kuna maendeleo ya vitu wakati wananchi walio wengi wanazidi kuathirika na mfumo uliopo wa kiuchimi; mabenki yapo lakini hakuna anayepata mkopo, soko limekuwa holela, vitu visivyokuwa na viwango vimejaa sokono, wakati bidhaa zetu zinakosa soko.
“Sekta zisizo rasmi, ambapo wanawake wengi ndio wapo huko haijaweza kumkomboa mwanamke na kumtoa katika duru ya umaskini. Ajira bado ni tatizo kubwa kwa wanawake Tanzania,” amesema Liundi.

Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Udhibiti wa Nishati, Maji na Mafuta, (EWURA), Felix Ngamlagosi akizungumza na waandishi wa habari (hawapo pichani).
Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Udhibiti wa Nishati, Maji na Mafuta, (EWURA), Felix Ngamlagosi akizungumza na waandishi wa habari (hawapo pichani).

EWURA yashusha tena bei ya mafuta

MAMLAKA ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA), inatangaza bei kikomo za bidhaa za mafuta ya petroli hapa ambazo zitaanza kutumika kuanzia Machi 4, 2015. Anaandika Mwandishi wetu… (endelea).
Kwa mujibu wa Mkurugenzi Mkuu wa EWURA, Felix Ngamlagosi, bei kikomo kwa rejereja kwa mkoa wa Dar es Salaam zitakuwa sh. 1,652 (petroli), 1,563 (dizeli) na 1,523 (mafuta ya taa) wakati bei kikomo za jumla ni sh. 1,547.19 (petroli), 1,457.58 (dizeli) na 1,547.19 (mafuta ya taa).
Ngamlagosi anasema bei za jumla na za rejareja kwa aina zote za mafuta, yaani, petroli, dizeli na mafuta ya Taa zimeshuka ikilinganishwa na bei katika toleo lililopita la Februari 4, 2015.
“Katika toleo hili, bei za rejareja kwa Petroli, Dizeli na Mafuta ya Taa zimepungua kwa viwango vifuatavyo: Petroli sh. 116/lita sawa na asilimia 6.57, Dizeli sh. 145/lita sawa na asilimia 8.49 na Mafuta ya Taa sh. 134/lita sawa na asilimia 8.08.,” amesema.
Aidha, kwa kulinganisha matoleo haya mawili, bei za jumla zimepungua kama ifuatavyo: Petroli, sh. 119.23/lita sawa na asilimia 7.16, Dizeli, sh. 147.94/lita sawa na asilimia 9.21, na Mafuta ya Taa, sh. 136.79/lita sawa na asilimia 8.80.
Kuendelea kushuka kwa bei za mafuta katika soko la ndani kumetokana na kuendelea kushuka kwa bei za mafuta katika soko la Dunia.
Mkurugenzi huyo anaongeza kuwa, bei za mafuta masafi (refined petroleum products) katika soko la dunia, kwa Petroli, Dizeli na Mafuta ya Taa zimepungua kati ya Julai 2014 na Januari 2015 kwa Dola 536/tani, Dola 400/tani na Dola 440/tani sawia sawa na punguzo la asilimia 53, 46 na 48 sawia.
“Kati ya Septemba 2014 na Machi 2015 bei za Petroli, Dizeli na Mafuta ya Taa katika soko la ndani zimepungua kwa jumla ya kiasi cha sh. 615/lita, sh. 528/lita na Sh 517/lita sawia ambayo ni sawa na punguzo la asilimia 27, 25 na 25, sawia,” amesema.
Katika kipindi husika, thamani ya shillingi ya Tanzania kulinganisha na dola ya Marekani ilishuka kwa asilimia 8. Bei ya mafuta kwenye soko la ndani ingeweza kupungua zaidi kama thamani ya shillingi isingeendelea kudhoofu.
Amesema kuwa kampuni za mafuta zipo huru kuuza bidhaa za mafuta ya petroli kwa bei ya ushindani ilimradi bei hizo ziko chini ya bei kikomo (price cap) kama ilivyokokotolewa na fomula iliyopitishwa na EWURA na ambayo ilichapwa kwenye Gazeti la Serikali Na. 354 la tarehe 26 Septemba 2014.
Chanzo cha mwanahalisi online

Baadhi ya maafa ya mvua yaliyotokea nchini
Baadhi ya maafa ya mvua yaliyotokea nchini

Mvua ya mawe Shinyanga yaua 38 na kujeruhi 60 

WATU 38 wamefariki dunia na wengine zaidi ya 60 kujeruhiwa vibaya kufuatia mvua kubwa ya mawe iliyonyesha usiku wa kuamkia leo na kusababisha mafuriko katika Kijiji cha Mwakata,  Kata ya Isaka Wilaya ya Kahama mkoani Shinyanga. Anaandika Mwandishi wetu… (endelea).

Awali, MwanaHalisi Online, ilikariri taarifa ya Mkuu wa Wilaya ya Kahama, Benson Mpesya, akisema kuwa mvua hiyo imeezua na kuharibu nyumba, kusomba mazao mashambani, mali, vyakula na mifugo.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Shinyanga, Justus Kamugisha amethibitisha tukio hilo lilitokea usiku wa Machi 3 mwaka huu, majira ya saa 3:00 usiku.
Kwa mujibu wa Kamugisha, watu 35 walifariki papo hapo huku majeruhi zaidi ya 60 wakikimbizwa Hospitali ya Wilaya ya Kahama kwa ajili ya matibabu. 
MwanaHalisi Online limeelezwa kuwa kati ya majeruhi 60 waliofikishwa hospitali, watatu walifariki wakati wakiendelea na matibabu.
Naye mganga mkuu wa hospitali hiyo, Joseph Ngowi, amesema kuwa idadi kamili ya watu waliojeruhiwa au kufa haikuwa imefahamika na kwamba wametuma madaktari kwenda kijijini hapo kwa ajili ya huduma.
Mkuu wa Wilaya ya Kahama, Benson Mpesya, amesema Kamati ya ulinzi na usalama ya wilaya imekutana kwa ajili ya kutathmini takwimu za uharibifu.
RAIS anayeondoka madarakani nchini Namibia, Hifikepunye Pohamba
RAIS anayeondoka madarakani nchini Namibia, Hifikepunye Pohamba

Huyu ndiye Rais Pohamba mshindi wa tuzo ya Mo Ibrahim

RAIS anayeondoka madarakani nchini Namibia, Hifikepunye Pohamba (79), ameingia kwenye historia ya washindi wa tuzo ya dola milioni tano ya Mo Ibrahimu ya uongozi wa Afrika.
Rais huyo ambaye anatarajiwa kumkabidhi madaraka yake kwa rais mteule, Hage Geingob, anakuwa kiongozi wan ne kukwaa tuzo hiyo, akitanguliwa na Joachim Chissano wa Msumbiji (2007), Festus Mogae wa Botswana (2008) na Pedro Pires wa Cape Verde (2011).
Tuzo hiyo ya dola milioni 5 hutuzwa kiongozi wa Kiafrika aliyechaguliwa na anayeongoza kwa njia bora na kuinua maisha ya watu na kuondoka madarakani.
Rais mtaafu wa Msumbiji mwaka 2005, Chissano ndiye alikuwa wa kwanza kutunukiwa tuzo hii ya heshima mwaka 2007, huku miaka mingine ikipita bila kupata mshindi kutokana ugumu wa vigezo.
Salim Ahmed Salim- Mwenyekiti wa kamati inayotafuta mshindi wa tuzo hiyo iliyotolewa Nairobi nchini Kenya, anasema Namibia chini ya Pohamba imeweza kuwa na utawala mzuri na kujiletea heshima. Anaongeza kuwa Namibia chini ya Pohamba ina demokrasia ya kweli, imekuwa imara na inayoheshimu uhuru wa habari na haki za binadamu,
Tuzo hii ni malipo ya awali ya dola za Marekani milioni 5 (sawa sh. bilioni 8.3) zinazotolewa kwa awamu kwa kipindi cha miaka kumi, zaidi ya malipo haya Pohamba atapewa dola laki 2 kwa kila mwaka kwa maisha yake yote.
Pia tuzo hii inaaminika kuwa kubwa na yenye thamani zaidi duniani ikiipiku Tuzo ya Nobeli ya Amani (Nobel Peace Prize) kwa zaidi ya mara tatu na nusu. Mshindi wa Tuzo ya Nobel anapewa kiasi cha dola za Marekani milioni 1.3.
Tuzo ya Mo Ibrahim inatolewa kwa Rais aliyemaliza muda wake Afrika na mchakato wa kumpata unafanywa na kamati maalumu ya watu mashuhuri; kamati hii pia inajumuisha watu wengine wawili waliowahi kupata tuzo ya Nobel.
WASHINDI
2007-Joachim Chissano (Msumbiji)
2008-Festus Mogae (Botswana)
2009- Hamna tuzo iliyotolewa
2010- Hamna tuzo iliyotolewa
2011-Pedro Pires (Cape Verde)
2012-Hamna tuzo iliyotolewa
2013-Hamna tuzo iliyotolewa
2014- Hifikepunye Pohamba (Namibia)
Tuzo hii inatolewa ili kutambua na kusherehekea viongozi wa Afrika waliotumia uwezo wao kuzijenga nchi zao kwa kuimarisha uchumi na huduma za kijamii na waliofanya juhudi za kupunguza umaskini na uimarishaji wa maendeleo endelevu yenye usawa kwa wote.
Utolewaji wa tuzo hii unaifanya Afrika iendelee kufaidika na uzoefu na weledi wa marais waliomaliza muda wao wa kutawala. Tuzo hii inawawezesha kuendelea kufanya shughuli nyingine za kijamii wanapomaliza muda wao wa kutawala.
Vigezo vinavyotumika katika kutafuta mshindi ni pamoja na Rais aliyemaliza muda wake katika nchi mojawapo ya Afrika; awe ameng’atuka madarakani sio zaidi ya miaka mitatu iliyopita; aliyechaguliwa kidemokrasia; aliyetumikia muda wake kwa mujibu wa katiba na aliyeonyesha kwa vitendo kuwa na sifa za pekee za uongozi.
Pohamba ni nani?
Huyu amezaliwa mwaka 1935 huko Namibia ya Kaskazini, eneo lililokuja kuwa ngombe ya harakati za SWAPO- Chama ambacho tangu uhuru 1990 kimekuwa kikitawala na kushinda chaguzi kwa ushindi wa kishindo.
Pohamba alipata elimu yake kwa wamisionari na akaajiriwa na mgodi wa Shaba akiwa kijana. Ni mwenza wa uanzilishi wa SWAPO na rafiki yake Sam Nujoma, aliyekuwa Rais wa kwanza wa Namibia.
Aliwahi kufungwa kwa sababu za harakati na utawala uliosaidiwa na makaburu. Amekuwa Waziri wa Ardhi baada ya uhuru, aliyeleta mabadiliko kwenye sekta ya ardhi ikiwa ni pamoja na kuigawa kwa wananchi.
Pohamba alipendekezwa na Nujoma kurithi mikoba ya urais mwaka 2004 na sasa mikoba hiyo anamwachia Hage Geingob.
Tuzo hii inafadhiliwa na Mo Ibrahim mzaliwa wa Sudan lakini ana uraia wa Uingereza; ni mjasiriamali na bilionea anayemiliki biashara ya mawasiliano ya simu kwakuwekeza katika nchi za Afrika.
Tuzo hii inatolewa kila mwaka lakini tangu 2007 ilipoanza ni marais watatu tu walizawadia, huku Nelson Mandera akizawadia kwa heshima.
Chanzo cha habari mwanahalisi online

Mwili wa Marehemu, John Damiano Komba
Mwili wa Marehemu, John Damiano Komba

Kapteni Komba afa na deni la CRDB

MBUNGE wa Mbinga Magharibi (CCM), John Komba, amefariki dunia kutokana na kuzongwa na mzigo wa madeni, likiwamo mkopo kutoka Benki ya CRDB.
Taarifa zinasema, benki hiyo ilitoa kiasi cha sh. 12 bilioni kwa mwanasiasa huyo mwaka 2009, lakini hadi mauti yanamkuta, alikuwa hajaweza kulipa deni hilo. Anaripoti Saed Kubenea…(endelea).
Habari zinasema, wakati Komba akihaha kuokoa nyumba yake kutokana na tanganzo la benki ya CRDB kwenye vyombo vya habari; huku akiwa tayari ameonekana kukata tamaa; ghafla Jumamosi jioni alipatwa na shinikizo la damu na kufariki dunia.
Mamilioni hayo ya shilingi yalitolewa na CRD Benki kwa mbunge huyo kwa ajili ajili ya kuendeleza shule zake mbili alizokuwa akizimiliki – shule ya Sekondari ya Bakili Muluzi na Shule ya Msingi ya Coletha – zilizoko jijini Dar es Salaam.
Hadi anafariki dunia, Komba alikuwa amebakiza kiasi cha zaidi ya sh. 78.5 milioni. Deni la Benki linatokana na mkopo pamoja na riba ya asilimia 17 katika kipindi cha miaka mitano ya uhai wa mkopo.
Komba amefariki dunia Jumamosi iliyopita, miezi mitatu baada ya Benki ya CRDB kuuza shule zake.
Mbali na kuuza shule, benki iliuza vifaa mbalimbali, likiwamo eneo la ukubwa wa mita za mraba zaidi ya 34,000 lililotumika kutoa mkopo wa sh. 900 milioni mwaka 2009.
Shule za Komba pamoja na vifaa vyake, vimenunuliwa na mfanyabiashara mmoja mmoja.
Gazeti hili limeelezwa kuwa Komba alijaribu, bila mafanikio, kushawishi serikali kununua shule yake; na kwamba alitinga hadi ikulu na makao makuu ya CCM kuomba msaada ili shule na nyumba yake visiuzwe.
Hata hivyo, taarifa zinasema, Komba hakufanikiwa kupata msaada wa kuzuia shule kuuzwa. Hadi anafariki dunia benki ilikuwa inajiandaa kuuza nyumba yake.
“Yule bwana alifika hadi ikulu kuomba msaada ili nyumba yake isiuzwe. Alitaka serikali imsaidie kununua shule yake; au kuomba benki izuie kwa muda uuzaji kwa kuwa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT) lilikuwa limekubali kununua eneo hilo kwa bei ya soko,” ameeleza mtoa taarifa.
Baada ya shule kuuzwa na deni kushindwa kumalizika, mtoa taarifa anasema, Komba alirudi tena ikulu na CCM kuomba msaada wa kukwamua nyumba yake.
Waziri Mkuu Mizengo Pinda, alijaribu kunusuru shule ya Komba kupigwa mnada kwa kuiandikia benki ya CRDB kumpa mwanasiasa huyo muda zaidi wa nyongeza ili kulipa deni lake.
Hata hivyo, pamoja na maombi ya Pinda kupewa nafasi, bado Komba alishindwa kulipa deni hilo.
Komba aliyekuwa anajulikana kwa jina maarufu la “Mzee wa kutoa mitaji kwa vimwana,” alizikwa juzi Jumanne, katika jimbo lake la uchaguzi la Mbinga Magharibi.
Chanzo cha habari mwanahalisi online