Monday, December 29, 2014

‘Operesheni Delete’ wabunge waliotetea Escrow bungeni yaiva


Wanasiasa wanaotajwa kuwa katika wakati mgumu wa kukubwa na kimbunga cha Escrow ni baadhi ya wabunge na mawaziri walioonekana waziwazi ndani ya Bunge kuunga mkono na kutetea uchotwaji huo haramu.
Duru za siasa zinaeleza kuwa tayari utaratibu wa kuwatambua wabunge wote waliounga mkono uchotaji huo imeanza miongoni mwa wanasiasa wenyewe.
Jambo hilo linaelezwa kufanywa pia na kambi ya upinzani Ukawa, ili kuanza mkakati maalumu utakaojulikana kama ‘Operation Delete Wabunge na Mawaziri Escrow’ itakayofanyika kwenye majimbo yote ya wabunge hao.
Hatua hiyo imeelezwa pia kuungwa mkono na wabunge wengine wa CCM waliosimama kidete kupinga na kukemea wizi huo hadi kupatikana  ushindi ndani ya Bunge lililomalizika hivi karibuni.
Wanaotajwa kuathirika zaidi ni mawaziri waliojifanya kuwatetea kwa nguvu watuhumiwa huku wakijaribu kupiga kila jambo hata lile lililoonekana kuwa lina ukweli kutoka kwenye Ripoti ya  Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali.
Katika kundi la wabunge waliopona kimbunga hicho wametajwa Stephen Wasira (Waziri wa nchi Ofisi ya Rais, Mahusiano na Utaribu), Profesa Mark Mwandosya (Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Kazi Maalumu) na  Mwigulu Nchemba (Naibu Waziri wa Fedha) ambao wanaungwa mkono hata na wapinzani kutoka na kuongoza mkakati wa kukemea mawaziri wenzao ndani ya CCM waliotuhumiwa kuchota pesa hizo.
Mawaziri wengi waliobaki wote wapo kwenye joto la kusimamiwa kidete  kuhakikisha wanang’olewa kwenye nafasi za ubunge majimboni kwao, ili kuwa funzo la kujali na kutambua maslahi ya taifa badala ya kutetea mambo na kuyachukuliwa kwa ushabiki wa vyama hata pale yanapokuwa na maslahi ya nchi.
Ni dhahiri kwamba wana CCM wa kweli wakiongozwa na Katibu Mkuu wa CCM, Abdulrahman Kinana na Katibu Mwenezi wa chama hicho, Nape Nnauye  wamefurahishwa na uamuzi wa Bunge na kusimama hadharani kutangaza kuunga mkono maazimiom hayo ya Bunge ya kuwaweka kando mawaziri hao kutokana na kashfa hiyo iliyotikisa nchi.
CCM imepita katika wakati mgumu kutokana na kashfa hiyo, hivyo wanakijua chama hicho na wanachama wake, wanatambua umuhimu wa kuenguliwa kwa mawaziri hao kama njia mojawapo ya kukisafisha chama wakati huo wa kuelekea uchaguzi wa Serikjali za mitaa na uchaguzi mkuu mwakani.
Wanatambua kwamba kashfa ya Escrow imeacha doa kwa chama hicho na endapo hazitachukuliwa hatua kali na za wazi kuwawajibisha watendaji hao, chama  hicho kinaweza kujikuta kwenye wakati mgumu na kuadhibiwa na wananchi kwenye masanduku ya kura.
Katika kutambua hili CCM yenye hazina kubwa ya viongozi na watendaji katika kada mbalimbali inaona kwamba haiweza kupoteza lolote kuwatosa mawaziri hao  na watendaji wengine waliotajwa kwenye sakata hilo,  ili ibaki heshima  na imani  yake kwa  umma wa Watanzania.
Kuna taarifa za uhakika kwamba wananchi kwenye majimbo ya wabunge waliojifanya kusimama na kutetea uchafu  huo, hawawahitaji tena wabunge hao na tayari kuna makundi makubwa ya watu kutoka Ukawa na hata ndani ya CCM yenyewe wameanza kunyemelea majimbio hayo huku wakiungwa mkono na wananchi baada ya wabunge wa zamani kupoteza ladha kwa kutetea sukari mbovu ya Escrow.
Ni dhahiri kwamba wanaiasa hao huenda kwa kutotambua au kusoma alama za nyakati walishindwa kujipanga kuona upepo ulipoelekea. Wabunge waliosimama kupinga wizi huo, wamepanda chati ghafla na  wanatajwa kutokuwa na hofu kwenye uchaguzi mkuu ujao kwenye majimbo yao.
Inaelezwa wananchi wao wametambua kwamba wabunge hao ni wawakilishi sahihi wenye mtazamo wa kizalendo katika kutetea masuala yenye malahi ya Taifa. Wana imani nao kuendelea kuongoza majimbo hayo. Wabunge kama akina Christopher Sendeka, Kangi Lugola, Deo Filikunjombe na wengine ndani ya CCM waliovaa ujasiri na kuweka kando ushabiki wa chama kukemea wizi wa Escrow wametajwa kuwa ni wabunge wasio na wasiwasi kurudu bungeni mwaka 2015.
Waliojivika kutokuelewa na kupiga kelele kutangaza uhalali wa uovu huo ambao mwisho wa siku bunge limebaini kuwa uliokuwa  ni wizi na uchafu na kukabidhi majina ya wahusika wakuu kwa Rais Kikwete kwa hatua zaidi, sasa hivi wanatembelea kwenye kamba nyembamba.
Wabunge hao wana nafasi ndogo ya kushinda, kwani tayari wameshaonekana udhaifu wao katika kuelewa  na kutetea masuala yanayogusa taifa. Hawa wote wametajwa kuwa orodha yao itaainishwa na kupelekewa wananchi wao, ili wawakatae kwani wana upofu wa kutojua maslahi ya Taifa na ni watetezi wa watu waliopotoka.
Hivyo siku za kulia na kusaga meno kwa wabunge na wa mawaziri waliotetea Escrow ndani ya mjadala wa Bunge, zinahesabika na adhabu yao hao hakabidhiwi Rais Kikwete, bali wananchi waliowachagua.

Tusipokemea rushwa tutaiangamiza nchi yetu


TANZANIA hivi sasa inakabiliwa na rushwa, ufisadi na matumizi mabaya ya madaraka ambayo kwa kiasi kikubwa yamechangia kusuasua kwa maendeleo.
Baaadhi ya Watanzania wenzetu wamekuwa na tabia ya kuwakejeli viongozi wanaosimama majukwaani kukemea vitendo viovu vya rushwa na ufisadi.
Tatizo la rushwa na ufisadi liliota pembe ndani ya Chama cha Mapinduzi (CCM), hususani pale ilipojitokea kashfa ya Richomond na kumwondoa madarakani aliyekuwa Waziri Mkuu, Edward Lowassa na viongozi wengine waandamizi wa Serikali wakimwemo mawaziri, Naziri Karamagi na Dk. Ibrahim Msabaha.
Rushwa na ufisadi ni mambo makuu mawaili yanayotajwa na Watanzania wengi kwamba yataiangusha CCM. Viongozi wengi wa CCM wamekuwa hodari wa kutaja rushwa, lakini matendo yao hayaendani na maneno yao. Hata hivyo kuna kundi lingine ndaninya CCM linaloona kuwa kutaja rushwa ni kama kuichuria mkosi CCM. Kundi hili pamoja na kujua kwamba rushwa na ufisadi upo halidiriki hata siku moja kwa ndimi zao kukemea na kutaja neno “rushwa” au “ufisadi”.
Kundi hili linaona kana kwamba kutaja neno rushwa au ufisadi ni kujidhalilisha bila kujua kwamba kufanya hivyo kwa vitendo , ndio kukijenga na kukitakia mema chama. Kumbukumbu zipo pale Waziri Mkuu mstaafu, Frederick Sumaye aliposimama hadharani na kukemea vitendo vya rushwa na ufisadi ndani ya  chama chake.
Kilichofuata baada ya hatua hiyo ya ujasiri, ni kiongozi huyo kupingwa  na hata viongozi wa juu wa chama, wakati huo Katibu Mkuu wa CCM akiwa Luteni mstaafu , Yusuf Makamba aliyemtaka  atumie vikao vya chama kuzungumza mambo hayo.
Tatizo linaloathiri CCM na huenda likahitimisha zama za uongozi wake ni woga wa viongozi wake kukikosoa chama na kutamka ukweli hadharani kama alivyokuwa akifanya Baba wa Taifa Mwalimu Julius Nyerere. Kuna viongozi wachache sana ndani ya CCM wenye uwezo wa kusimama na kukosoa chama au serikalipale inapokwenda ndivyo sivyo, mfano mmojawapo wa viongozi hao, ni pamoja na Katibu Mkuu wa sasa wa CCM,  Abdulrahman Kinana.
Rushwa  iliponuka ndani ya CCM na baadhi ya viongozi wake kuonekana kero kwa umma na kuanza kukipoteze umaarufu chama hicho, kilianzisha mkakati wa kujivua gamba. Mkakati huo ulioanzishwa na aliyekuwa Katibu Mkuu wa CCM , Wilson Mkama ulikuwa  tiba kamili ya kuiponya CCM  na kuiepusha na viongozi wasiofaa, wala rushwa na mafisadi na hata wale wanaotajwa tajwa tu, bali kwa nia njema ya kukinusuru chama, ulikwama matokeo yake Mkama kujikuta akiwa mhanga mwenyewe kwa kuenguliwa kutoka nafasi hiyo.
Viongozi wengi wa CCM huenda ni kwa kulewa madaraka au kiburi tu, hawajitambui hususani pale wanapotembea kwenye ‘reli ya rushwa au ufisadi’. Viongozi hao wamekuwa ni mioyo migumu kama ule wa aliyekuwa mtawala wa Misri Farao, kujiuzulu kwa kosa lolote hata pale wanapohisiwa tu. Kuna hisia mbaya  ambazo wakati mwingine zinakuwa hazina ukweli, lakini kwa kiongozi madhubuti mwenye maadili ya dhati, haoni shida kujiuzulu wadhifa wake hata pale tu anapohisiwa.  Huo ndio usafi wa viongozi wenye nia na dhamira ya dhati kutumikia umma.
Tumeona  mifano ya namna viongozi wa dola nchini Kenya walivyojiuzulu akiwemo Mkuu wa Jeshi la polisi la nchi hiyo kutokana na matatizo ya kiusalama . Tukiangalia mfano huo mwema tunaoanisha na viongozi wetu hapa nyumbani  ambao hivi karibuni walizua mtafaruku mkubwa ndani ya Bunge kiasi cha kutaka kumponza Waziri Mkuu, Mizengo Pinda kuachia nafasi yake. Viongozi hapo pamoja na mapendekezo ya kiungwana kabisa ya wabunge wa pande zote chama tawala CCM na wale wa upinzani kuwataka waachie kazi, bado wanasubiri eti mpaka  Rais awaachishe kazi!
Inasikitisha! Kwa kiongozi muungwana mtafaruku unapofikia kiwango cha juu kama ilivyotokea ndani ya mkutano wa Bunge uliomalizika hivi karibuni, hana sababu ya kusubiri eti akabidhiwe kwa mamlaka ya juu ili imwajibishe, ni wajibu wake kufanya hivyo hata kama hakufanya kosa hilo, lakini zogo pekee ndani ya Bunge linatosha kumfikisha kwenye maamuzi ya kujiuzulu, ili kulinda heshima yake na umma wa Watanzania kwa ujumla.
Kujiuzulu kwa wanasiasa ni heshima na kielelezo cha maadili mema ya utumishi wa umma, sio kusubiri utolewe ndani ya chumba wakati unaona umesabaisha ‘moshi wa kutisha’ na ili chumba kiwe salama ni wewe kutoa nje, bado unang’ang’ania.  Hapa tunapata picha na kilelezo thabiti kwamba tuna viongozi wa namna gani ambao hawawezi hata kumhurumia Rais wetu mpendwa ambaye hivi karibuni ametoka hospitali kwa matibabu makubwa.
Watu wa namna hii wanamjaribu nini Rais wetu? Rais ana watu wengi na Tanzania ina hazina kubwa ya watendaji wenye uwezo wa kutukuka na kamwe mtu mmoja hawezi kuwa bora kuliko watu wengine. Njia bora ya kiungwana ni kuchukua hatua ya kuondoka mapema kabla ya kusubiri maka Rais akuambie kufanya hivyo.
Viongozi shupavu wa kukemea rushwa kama Sumaye na wengine akina Kinana na Katibu Mwenezi wa CCM, Nape Nnauye,  wameuwa wakiimba juu ya tatizo la rushwa kila wakati, lakini  baadhi ya watendaji hawasikii. Mfano Sumaye karibu kila hotuba yake amekuwa akikosoa na kuonya kuhusu rushwa na ufusadi, badala ya viongozi kutuliza masikini na kutafakari hayo baadhi wanaishia hata kudhihaki maneno yake.  Kinachotia moyo ni kwamba mtu mkweli daima huwa hachoki kusema  kupigania na kusimamia kile anachoona ni kweli.
Viongozi wetu wangekuwa watu wenye kujali na kusikia maneno kama hayo naamini haya yaliyotokea ya viongozi kuchota mapesa kwa ‘lumbesa’ yasingetokea. Inasikitisha kwamba watu wa kunena na wenye maono tunao, wanaonya na kukemea lakini watu wana macho  lakini hawaoni, wana masikio lakini hawasikii, matokeo yake ni kuwa na  vongozi wa ovyo wanaoingia au kuhusishwa na mambo machafu kinyume cha maadili ya viongozi.
CCM ifike mahali sasa ikubali kukosolewa kujikosoa na kuwapa nafasi viongozi wake wanaikosoa, ili kuonyesha njia sahihi na mwelekeo wa chama badala ya kubeza wakati kuna tatizo linalotengeneza ‘kansa’ kubwa ndani ya chama.  Kama maneno ya akina Sumaye na akina Nape yasingebezwa ndani ya chama, CCM ingekuwa na viongzi waadilifu wenye miguu ya kusimama mbele ya Watanzania bila mashaka.
CCM inapokwenda kutafuta mgombea wake mwaka 2015 izingatie suala la usafi  wa kiongozi, uwezo na ujasiri wake wa kukemea, kuonya na kuonyesha mwelekeo wa maadili ndani ya chama , taifa sambamba na kujenga uchumi imara.

Dk. Slaa: Acheni kulalamika

  • Ataka Watanzania kuchukua maamuzi magumu
  • Asema dawa ni kuiondoa CCM, si kubadili viongozi
Dk. Slaa: Acheni kulalamikaKATIBU Mkuu wa Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Dk. Willibrod Slaa, amewataka Watanzania kuacha kulalamika baadala yake wachukue maamuzi magumu ya kutokichagua Chama Cha Mapinduzi (CCM), ambacho kimebobea kwa rushwa.
Kauli hiyo aliitoa mwishoni mwa wiki jijini Dar es Salaam katika ‘Operesheni Amsha Amsha Mzizima’, kuelekea Uchaguzi wa Serikali za Mitaa unaotarajiwa kufanyika Desemba 14 mwaka huu.
Dk. Slaa, alisema kwamba katika kipindi cha miaka 53, CCM imeshindwa kuwaletea maendeleo ya kweli na baadala yake imekuwa ikiwanyonya wanachi kutokana baadhi viongozi wake kuendekeza rushwa katika kila huduma za kijamii.
“Viongozi wote wa CCM kuanzia ngazi ya kitongoji ni wala rushwa, mfano ni pale mtu anapotaka hata kuwekewa saini kwenye barua na Mwenyekiti wa Kitongoji au Mtaa anatakiwa atoe rushwa na kwa upande wa vigogo ndio balaa,” alisema Dk. Slaa.
Dk. Slaa, aliongeza kuwa, CCM ni chama cha rushwa kwa sababu hakuna mahali popote hapa nchini mtu anaweza kupata mkopo bila kuwa na kadi ya CCM, kitendo ambacho kinawanyima baadhi ya wananchi haki.
“Tatizo la CCM sio la mtu mmoja mmoja ni tatizo la mfumo wa Chama hicho na halitaondolewa kwa kubadilisha viongozi, bali litaondoka kwa kubadilisha mfumo mzima hususani kuwachagua viongozi wa Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa).
“Watanzania ni walalamikaji na wanung’unikaji sana, lakini uamuzi upo mikononi mwenu… miaka 53 bado mnachagua mapanya, ukiweka chakula chako kwenye gunia la mchele hukuweka Paka, akiingia Panya anakula nusu kila gunia,” alisema Dk Slaa.
Alisema nchi haisogei mbele kutokana na watu wachache ambao ndio wanaopata kihalali huku akidai kuwa, mwaka 2007 hata Rais Kikwete alikuwepo miongoni mwa waliohusika na suala la Kampuni ya IPTL.
“CCM haina ‘shoo’ tena ya kubadilisha nchi, miaka 53 hakuna kipya kilichotokea, kuanzia sasa michango ya kipuuzi kama michango ya mwenge tunaipiga marufuku, mwenge wa Nyerere ulileta maendeleo, lakini mwenge wa Kikwete ni chanzo cha mambukizi ya ugonjwa hatari wa Ukimwi,” alisema.
Naye Diwani wa Sinza, Renatus Pamba (CHADEMA), alisema mwaka 2010 wakati wanaingia madarakani, katika Manispaa ya Kinondoni walikuta mapato ya ndani yalikuwa sh bilioni 4, lakini wameweza kuziba mianya yote ya upotevu wa fedha, hali iliyofanya mapato hayo kuongezeka na kufikia sh bilioni 36 hadi sasa.
Alisema hatua walizochukuwa ni kufuta mihuri yote ya wenyeviti wa serikali za mitaa na kuandaliwa ya maofisa watendaji, na walifanya hivyo kwa sababu mihuri hiyo ilikuwa ikisababisha migogoro ya ardhi.
Kwa upande wake, Maulidi Mkandu, ambaye ni mgombea wa nafasi ya uenyekiti kupitia CHADEMA katika mtaa wa Mnazi Mmoja Manzese Tip top, alisema katika mtaa huo wanakabiliwa na matatizo mbalimbali ikiwemo uchafu, michango ya sungusungu na ujenzi wa maabara ambayo yamesababishwa na CCM kwa kuwa wabadhirifu wa fedha na kutoweka wazi mapato ya umma.
“Kama mtaniweka madarakani nitahakikisha nawafichua wabadhirifu wa fedha, hapa kuna tatizo la taka ngumu, sungusungu na maji, hatuelewi mapato yanapelekwa wapi, nawahakikishia kuwa nitafuatilia mapato na nitakuwa muadilifu,” aliwahikishia wananchi.

Utamu wa madaraka unazamisha nchi

MIAKA ya nyuma kulikuwa na kitabu kimoja cha hadithi chenye hadithi ya kusisimua ya “Muwa uliozamisha Meli” kilichoelezea Manaodha wa meli walionogewa na utamu wa muwa waliokuwa wanakula ndani ya meli kiasi cha kusahau kuongoza meli hadi ikazama.
Manahodha hawa wanafanana na viongozi wetu wa leo wanaoliongoza taifa letu na kushika nyadhifa nyeti wanaonekana kunogewa na utamu wa madaraka kiasi cha kutowajibika na kuizamisha nchi katika dimbwi la umasikini, upotevu wa rasilimali za nchi, huduma mbovu za kijamii bila kujali.
Fahari za uongozi, magari ya kifahari, posho lukuki na bahasha za bashasha zimewavua uzalendo na uwajibikaji wamebaki watupu, wameishiwa japo ni waheshimiwa.
Wamekua waking’ang’ania na kupigania, kutetea utamu wa uongozi kuliko kuwatetea wananchi na kulinda maslahi ya nchi, jambo ambalo linazidi kuizamisha meli ya Tanzania.
Ili kuendelea kufaidi utamu huu, wamewaka mifumo ya kulindana na kubebana na kutengeneza makundi ndani ya vyama vyao vya siasa, ili wabaki kuwa juu zaidi pasiwepo na kuwashusha hata kama wanaizamisha nchi.
Viongozi hawa wanafurahia na kuona fahari ya utamu wa viongozi kuliko kuwatumikia wananchi. Uongozi kwao si mzigo bali ni dili ni sehemu ya kutajirikia.
Ni wazi kuwa manahodha kama hawa wataendelea kuizamisha Tanzania yetu kama wataendelea kuachiwa uskani ilhali wako bize wanakula muwa wameshasahau uskani wao. Hawajui hata ulipo sijui wamewaachia wawekezaji, matajiri na wafanyabiashara.
Siku zote utamu ukizidi unakua sumu, Waingereza wanasema “too much of everything is harmful” utamu huu unageuka sumu na kuuwa maadili ya uongozi, uwajibikaji, usimamizi wa rasilimali za nchi unakua mbovu kwa sababu kila mtu anataka utamu.
Utamu huu wa madaraka umesababisha ulevi wa madaraka, kulewa kiasi cha kutojali wananchi ambao kibiashara ama kimtaji wanaitwa wapiga kura.
Ulevi huu ukizidi unasababisha uteja wa uongozi, kiongozi anaona kuwa hawezi kuishi bila kuwa kiongozi kwa sababu ya utamu wanataka kuwa viongozi mpaka kufa, yuko tayari kung’ang’ana kwa gharama yoyote hata kama amelisababishia taifa hasara.
Uongozi wa namna hii unafananishwa na hotcake  umesababisha watu wawe na uroho wa madaraka na uchu usiopimika hawako tayari kuukosa wanaupigania kwa gharama yoyote hata kwa rushwa, mbinu chafu, umwagaji damu, kuchakachua na aina zote za udanganyifu wanazozijua.
Utamu wa madaraka unawazidia viongozi mpaka wanasahau kuwa wameshikilia uskani wa nchi, nchi inakosa mwelekeo matokeo yake inaanza kuzama polepole.
Ulevi huu wa madaraka umesababisha athari nyingi viongozi kufanya maamuzi ambayo yanaligharimu taifa kwa kiasi kikubwa mfano msamaha wa kodi kwa wawekezaji wanaovuna mabilioni ya rasilimali za watanzania na kuhodhi mamilioni ya hekari ilhali mmachinga analipa kodi licha kipato chake kidogo.
Utamu wa madaraka umewasahaulisha viongozi wengi wajibu na majukumu waliyonayo kwa nchi kiasi cha kuufanya uongozi uonekane kuwa ni ulaji ambao umekua ni dawa ya usingizi inayowafanya viongozi walale fofofo, wajisahau.
Viongozi wamelemewa na utamu wa uongozi hawataki kubeba jukumu la kujiwajibisha wala kuwawajibisha wengine kwa manufaa ya wananchi.
Kumekua na vitendo vingi vya ubadhirifu, ufisadi na wizi wa fedha za walipa kodi, lakini viongozi hawataki kuwajibika wamenogewa na utamum bora nchi izame waendelee kufaidi utamu.