Baadhi ya maafa ya mvua yaliyotokea nchini
Mvua ya mawe Shinyanga yaua 38 na kujeruhi 60
WATU 38 wamefariki dunia na wengine zaidi ya 60 kujeruhiwa vibaya kufuatia mvua kubwa ya mawe iliyonyesha usiku wa kuamkia leo na kusababisha mafuriko katika Kijiji cha Mwakata, Kata ya Isaka Wilaya ya Kahama mkoani Shinyanga. Anaandika Mwandishi wetu… (endelea).
Awali, MwanaHalisi Online,
ilikariri taarifa ya Mkuu wa Wilaya ya Kahama, Benson Mpesya, akisema
kuwa mvua hiyo imeezua na kuharibu nyumba, kusomba mazao mashambani,
mali, vyakula na mifugo.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Shinyanga,
Justus Kamugisha amethibitisha tukio hilo lilitokea usiku wa Machi 3
mwaka huu, majira ya saa 3:00 usiku.
Kwa mujibu wa Kamugisha, watu 35
walifariki papo hapo huku majeruhi zaidi ya 60 wakikimbizwa Hospitali ya
Wilaya ya Kahama kwa ajili ya matibabu.
MwanaHalisi Online limeelezwa kuwa kati
ya majeruhi 60 waliofikishwa hospitali, watatu walifariki wakati
wakiendelea na matibabu.
Naye mganga mkuu wa hospitali hiyo,
Joseph Ngowi, amesema kuwa idadi kamili ya watu waliojeruhiwa au kufa
haikuwa imefahamika na kwamba wametuma madaktari kwenda kijijini hapo
kwa ajili ya huduma.
Mkuu wa Wilaya ya Kahama, Benson Mpesya,
amesema Kamati ya ulinzi na usalama ya wilaya imekutana kwa ajili ya
kutathmini takwimu za uharibifu.